Kuku wa kienyeji ni wazuri kwa ufugaji kwa sababu: Wanavumilia sana
magonjwa, Ni rahisi kuwahudumia, Chakula chao ni cha bei ya chini,
Wavumilivu wa hali tofauti za hewa, Hawahitaji uangalizi wa karibu, na
soko lake ni kubwa sana na bei nzuri (Mayai trei moja SHs 10,000 mpaka
15,000, kuku wakubwa wanaanzia SHs 15,000 mpaka 30,000). Hii haimaanishi
kwamba, uwaache kuku bila uangalizi, kwani nao hupata magonjwa kama
wasipo patiwa chanjo sahihi, hupungua uzito na uzalishaji mayai hushuka
kama wasipo patiwa chakula chenye virutubisho vyote. Hapa naelezea vitu
muhimu katika hii formula ya ufugaji kuku wa kienyeji kwa mafanikio:
1. Aina ya kuku: Chagua aina ya kuku wenye uwezo wa
kutaga mayai mengi na wakati huohuo, kuzalisha nyama nyingi. Hii itakupa
faida kote, kwenye upande wa nyama na upande wa mayai. Kuku hawa
wanajulikana kama Chotara, wanatabia sawa na kuku wa kienyeji wenye
asili ya Tanzania wanaopatikana maeneo mengi nchini; kutokana na
uvumilivu wao wa magonjwa na hali tofauti za mazingira. Pia wanauwezo wa
kutaga mayai mengi (Wastani wa mayai matano kwa wiki) karibu sawa na
kuku wa kizungu. Aina ya kuku hawa ni kama vile, Chotara wekundu (Rhode
Island Red), Black Australorp (Weusi/Malawi), Barred Plymouth Rocks
(Madoa), New Hamshire Red, Kuroila wanapatikana sana Uganda, na Kari
kutoka Kenya. Hizi ni aina ya kuku zinazo patikana Tanzania.
2. Banda: Kuku wa kienyeji pia, wanahitaji banda au
nyumba ya kuku imara ili kuweza kuwakinga na baridi kali, wanyama
hatari, na wizi. Banda pia liwe na semu nzuri za kutagia na sehemu za
kulala ziwe juu , kwani kuku hupendelea kulala juu. Ni muhimu banda liwe
katika hali ya usafi muda wote. Kwa hivyo ni vizuri linyanyuliwe juu
kidogo ili kuruhusu uchafu kuanguka chini na lijengwe ka kutumia mbao,
mabanzi, milunda, nyavu, na mabati. Vifaranga wanahitaji kutenganishwa
na kuku wakubwa. Banda si lazima liwe la gharama kubwa, kwani mafanikio
ya ufugaji wa kuku ni vile unavyo waangalia na si banda. Mada inayohusu
mabanda bora ya kuku itakuja hivi karibuni.
3.Chanjo: Kama nilivyosema mwanzo, kuku wa kienyeji ni
wavumilivu wa magonjwa lakini si kwamba hawayapati, kuna magonjwa ambayo
ni hatari pia kwa kuku wa kienyeji. Chanjo ni muhimu kuwaepusha na
hatari ya kuyapata magonjwa haya. Chanjo muhimu kwa kuku wa kienyeji ni;
New Castle, Gumboro, Marek’s na Ndui ya kuku. Fuata utaratibu wa chanjo
kutokana na ushauri wa daktari. Nitawaletea pia makala ya magonjwa na
chanjo hivi karibuni. pia unaweza kutumia majani ya mpapai kuwachanja kuku wako.
4. Majogoo kwa majike: Ili mayai mengi yaweze kutotolewa,
ni vizuri jogoo mmoja aweze kuwahudumia majike wasio zidi 7. Kwani kuku
wanaweza kutaga bila ya jogoo, lakini mayai hayatoweza kuleta kifaranga.
Ili mayai yalete vifaranga ni lazima yawe yamerutubishwa (Fertilized
eggs) na jogoo. Kwa hivyo ni vizuri kuweka Jogoo 1 kwa majike5,
hivyohivyo Jogoo 2 majike 10, Jogoo 3 majike 15, n.k. Pia hakikisha kuku
wanao tumika kuendeleza kizazi ni wale wenye afya bora.
5. Vyombo vya chakula: Hakikisha vyombo vya chakula ni
visafi na vinawatosheleza kuku wote. Vyombo hivi ni vizuri vifanyiwe
usafi wa mara kwa mara, ili kuwaepusha kuku na magonjwa. Maji machafu
huwa ni chanzo kikuu cha magonjwa hasa ya kuhara. Hakikisha kuku wako
wanabadilishiwa maji angalau mara mbili kwa siku.
6. Chakula: Kuku wa kienyeji pia wanahitaji mchanganyiko
sahihi wa chakula, ili waweze kukupatia mazao mengi na bora, na
kuwaepusha na magonjwa. Zipo fomula mbalimbali za chakula kutokana na
umri wa kuku, na aina ya kuku. Kuku wote wanahitaji chakula chenye
mchanganyiko sahihi wa Madini, Vitamini, Protini, Fats, Wanga, Vyakula
vya kulinda mwili ili usipatwe na maradhi, na Maji safi. Muhimu
kuwapatia kuku majani kama ziada ya chakula, hii hupunguza gharama za
chakula na kuwafanya kuku waonekane wenye afya bora. Ni vizuri kuwapatia
vifaranga chakula spesheli cha dukani kama huna ujuzi wa kutengeneza
mwenyewe. Kwani vifaranga wengi hufa kutokana na kutokupata chakula
chenye mchanganyiko sahihi kwao. Kuku wa mayai pia wanahitaji
mchanganyiko sahihi ili waweze kutaga mayai kwa wingi.
Kuchagua aina/mbegu
Kuchagua mbegu inamaanisha: Mtetea au
jogoo mwenye ubora wa hali ya juu , akiwa na sifa kama uzalishaji wa juu
wa mayai au uzalishaji wa nyama, wanachanganywa na aina mfugaji
alionayo, au kuboresha mbegu ambayo ni dhaifu. Kuna makundi matatu ya
aina za kuku;
• Kuku wenye umbo dogo ni wazuri zaidi kwa uzalishaji wa mayai.
• Kuku wenye umbo kubwa ni wazuri zaidi kwa uzalishaji wa nyama.
• Mbegu iliyochanganywa ni nzuri kwa uzalishaji wa mayai na nyama.
Endapo mfugaji anataka kufuga kuku kwa
ajili ya mayai, basi anaweza kuchanganya mbegu ya kienyeji aliyonayo na
mbegu yenye umbo dogo ambao wana historia nzuri ya uzalishaji wa mayai,
na kama anataka kuzalisha kwa ajili ya nyama, basi anaweza kuchagua
wenye umbo kubwa. Na ambae anahitaji kwa ajili ya mayai na nyama, basi
anaweza kuchanganya mbegu.